Thursday, 14 August 2014

Sitta: Hatuwezi kusitisha mikutano Bunge la Katiba


Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta akizungumza na wafugaji kutoka mikoa mbalimbali nchini walipomtembelea ofisini kwake Dodoma jana. Wafugaji hao walipelekwa bungeni hapo na Mjumbe wa Bunge hilo ambaye pia ni Mbunge wa Maswa Magharibi, John Shibuda (kushoto). Picha na Emmanuel Herman  

Dodoma. Mwenyekiti wa Bunge la Katiba, Samuel Sitta amesema mikutano ya Bunge hilo haiwezi kusitishwa na kwamba itaendelea kwa kuwa idadi ya wajumbe waliopo inakidhi matakwa ya kisheria kutunga Katiba.
 Kadhalika Sitta amewatuhumu wajumbe wa wanatokana na kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kwamba si wazalendo kutokana na kususia Bunge hilo tangu Aprili 25, mwaka huu.
Akizungumza na wafugaji kutoka mikoa mbalimbali nchini walioongozwa na Mbunge wa Maswa Magharibi (Chadema), John Shibuda waliopeleka
mapendekezo yao ili yaingizwe kwenye rasimu ya Katiba, Sitta alisema wanaotaka Bunge hilo liahirishwe ni watu wasiolitakia mema Taifa.
“Lakini napenda kuwaambia kuwa Bunge la Katiba liko hapa kisheria kwa kanuni zake linaendelea na wale wanaopiga kelele lisiendelee ni watu ambao hawatutakii mema,” alisema Sitta na kuongeza;
“Kwa sababu demokrasia yoyote ni kupata kura za wengi, walioko hapa wanatosha kabisa kuendelea na mchakato huu mpaka mwisho wake kwa sababu tunaamini wakati wa Katiba Mpya umefika.”
Kauli ya Sitta imekuja siku moja tangu viongozi wa Ukawa unaojumuisha vyama vya NCCR-Mageuzi, Chadema na CUF watangaze kwamba wataitisha maandamano nchi nzima kushinikiza kusitishwa kwa Bunge hilo kwa maelezo kwamba ni matumizi mabaya ya fedha za umma iwapo Bunge hilo halitasitishwa.
Kadhalika, baadhi ya wabunge wa CCM wamesikika wakitaka Bunge hilo liahirishwe ili kunusuru fedha zinazotumika kugharamia shughuli zake, kwani hakuna uhakika wa kupatikana kwa theluthi mbili ya kuwezesha Katiba hiyo kupatikana.
Sitta alisema hakuna ubishi kwamba baadhi ya wajumbe walitoka ndani ya bunge hilo na kwenda nje ambapo wamekuwa wakipiga kelele na kwamba wao (waliobaki bungeni) ambao wana uzalendo lazima wahangaike nayo mpaka iweze kupatikana.
Alisema upungufu uliopo katika Katiba ya sasa, ndiyo unaofanya kutotungwa kwa sheria bora ambazo zitawezesha maslahi ya makundi mbalimbali yapatikane bila kuleta migongano kama iliyopo sasa.
“Ndio maana sisi tunasema kung’ang’ania suala la muundo wa serikali ni kwenda pembeni kidogo na matarajio ya watu. Huu ni ushahidi dhahiri kabisa kuwa lililo muhimu ni haki za raia,” alisema.
Alisema hata kama Katiba itakuwa na muundo wa serikali kwa idadi yoyote, ikiwa haitazingatia haki za makundi kama wafugaji, haitakuwa na maana.
Sitta alisema wanaifanyia kazi Katiba hiyo na kuwa itakuwa bora zaidi kushinda nyingine zilizopo katika nchi jirani.
Shibuda akandia Ukawa
Kwa upande wake Shibuda ambaye pia ni alijiita mlezi wa wafuhaji, aliwakandia Ukawa akisema wamekuwa wakitanguliza maslahi binafsi badala ya maslahi ya Wananchi huku akimpongeza Sitta kwa jitihada za kuendeleza mchakato wa Katiba.
“Napenda vile vile kukupongeza kwa jitihada zako za kuendeleza mchakato huu, pia nikupe pole kwa visirani vya kusigana vinavyotokea,” alisema Shibuda ambaye hata hivyo hakutamka moja kwa moja iwapo amerejea kushiriki vikao vya Bunge Maalum.
Alipoulizwa kuhusu suala hilo alisema: “Subirini mtaona yatakayojiri”.
“Wafugaji na wakulima wa pamba wanalaani na kusikitika kwamba Bunge hili linaacha kujadili matatizo yanayoikabili jamii badala yake ajenda muhimu inakuwa mfumo wa madaraka,” alisema na kuongeza;
“Hivi serikali tatu inatiririsha nini kwa wakulima? Serikali mbili inatiririsha nini kwa wakulima na wafugaji? Tunataka uongozi wa kukabiliana na matatizo ya wananchi, sio uongozi wa kukimbia matatizo ya wananchi.”
Shibuda alisema wakulima na wafugaji wanahitaji siasa iwe ni rufaa ya kujenga maendeleo ya jamii na kujengwa ukombozi wa Watanzania.
Shibuda alisema wao hawatakubaliana na watu wanaotaka kukuza umaarufu binafsi.
“Mimi nitapingana na mtu yoyote, nitakwenda kwenye jamii, nitakuja kwenu wafugaji nitakwenda kwa wakulima wa pamba ambao mimi ni mlezi wao, tutashauriana tukatae kutumiwa na kuburuzwa na maslahi ya watu wanaotaka kujikweza kwa maslahi binafsi,” alisema.
Alisema wakulima na wafugaji hawakubaliani na kauli za kibabe za watu wachache ambao wanategemea kutoa uhuru wa maoni yao kutegemea Katiba ya nchi lakini wakitofautiana mitazamo wanaanza kuwa wababe wanaoitwa chinjachinja kwa watu ambao wanatoa mawazo mbadala.
“Mheshimiwa (Sitta) wasikutishe kwa dhamira yako njema ya kuongoza vikao, hakuna chema kisicho na kasoro, mtu kama ana dhamira njema akiona kasoro akusahihishe kwa lugha ya kistaarabu kwa maslahi ya kusonga mbele,” alisema.

Akisoma mapendekezo ya wafugaji hao, Mwenyekiti wa Chama cha Wafugaji wa Kanda ya Magharibi, Kasundwa Wamarwa alisema wanatambau kuwa Bunge hilo litawapatia Katiba inayowatambua wafugaji wa asili.
“Kwa kauli moja sisi wafugaji hatutakuwa tayari kuipokea rasimu ya Katiba ambayo haitatambua mfugaji wa asili,” alisema.
Alisema njia kuu ambayo wanaamini itakuwa suluhisho ya matatizo yao ni Katiba Mpya huku akisema wajumbe wa Bunge la Katiba wanapaswa kuwa na hofu ya Mungu wakati wanapoendelea na mchakato huo.
“Tunawataka wajumbe wa Bunge la Katiba kukumbuka kuwa Katiba bora ni ile itakayotokana na maridhiano na utashi wa kisiasa,” alisema. Chanzo MWANANCHI


0 comments:

Post a Comment