UPO uwezekano mkubwa – kama kwa lazima au kwa kukosa njia nyingine – mchakato wa Katiba mpya utasitishwa.
Uwezekano
huu upo kwa sababu ya kutokuwapo maridhiano yenye kuwezesha majadiliano
kuendelea katika Bunge Maalumu la Katiba kufikia uandikwaji wa Katiba
inayopendekezwa.
Uwezekano wa kusitishwa kwa mchakato huu umepata
nguvu zaidi siku za karibuni hasa baadhi ya wanasiasa kutoka chama
tawala wanapotoa mawazo ya kutaka mchakato huu usitishwe hasa kwa vile
hakuna maridhiano kati ya wajumbe wanaotokana na Chama cha Mapinduzi
(CCM) na wale wanaotokana na wajumbe wa kundi la UKAWA lenye kujumuisha
vyama vikuu vya upinzani nchini kama CUF, CHADEMA, na NCCR Mageuzi.
Kama hili ni kweli – na ninaamini lina ukweli – basi ni lazima tujiulize na kutafuta jibu au majibu ya ni nini kinapaswa kutokea endapo mchakato huu utasisishwa.
Ni muhimu kujua mambo mbalimbali yanayopaswa kutokea ili tusije kujikuta tunarudia tena gotagota hii miaka michache ijayo.
Mchakato usiahirishwe, usitishwe tuanze moja
Jambo
la kwanza na la msingi endapo uamuzi wa kusitisha mchakato huu
utachukuliwa ni kuhakikisha kuwa uamuzi wowote hautakuwa wa kuahirisha
kama vile kuahirisha kikao cha Bunge la Muungano au Baraza la
Wawakilishi.
Kuahirisha kwa namna fulani itakuwa ni sawa na
kukubali kwa kiasi fulani yale yaliyotokea na kuwa tutaendelea “kuanzia
tulipoishia”.
Kwa maoni yangu, mchakato huu ulivurugwa tokea mwanzo kabisa na hivyo hata kuukubali kwa kidogo ni kuupa heshima isiyostahili.
Ni
vizuri basi uamuzi uwe wa kuufuta kabisa na kile kilichokwenda kwa
mganga (kilicholiwa) tukubali kuwa kimeliwa kwa sababu ya ubishi na
kiburi chetu kama Taifa.
Tuufute mchakato huu na kuacha uongozi
ujao au vizazi vijavyo vianzishe mchakato wao. Sisi tumejaribu pamoja na
elimu na ujuzi wetu lakini ndiyo tumeboronga hivi labda kipo kizazi cha
wenye weledi, akili, uzalendo na fikra bora ambacho kitafuata njia
sahihi za kuelekea Katiba mpya.
Tusubiri tuone kuelekea kampeni
za uchaguzi ni chama gani au vyama gani vitakuja na ajenda inayoeleweka
kuhusiana na Katiba mpya.
Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ifutwe
Kwa
vile mchakato huu umekuwa ukiendeshwa kwa kufuata ile sheria mbovu ya
Mabadiliko ya Katiba, basi hakuna njia nyingine ya kuusitisha isipokuwa
kwa kufutilia mbali sheria ile ambayo ilitungwa ikiwa inapingana na
Katiba ya sasa kwa asilimia 100. Nimeshawahi kuonyesha jinsi mchakato
huu ulivyokuwa haramu na sehemu mojawapo ya uharamu huo ni hii sheria.
Ni
vizuri basi hoja itakapotolewa kuusitisha mchakato huu wabunge wetu wa
Bunge la Muungano wajiandae kuleta mswada wa sheria itakayofutilia mbali
sheria hii na hivyo kuhakikisha kuwa mchakato huu unakufa kifo cha
asili ili tusije kuwaachia viporo na mabaki yanayonuka wale wanaotaka
kuja na kuanzisha mchakato mpya wa katiba mpya.
Hatima ya Muungano iamuliwe kabla ya Katiba mpya
Hili
likitokea – kufutiliwa kwa mchakato huu- mambo ya msingi sasa ni lazima
yashughulikiwe mapema iwezekanavyo ili angalau kwa kiasi kikubwa
kupunguza kazi huko mbele.
Baadhi ya mambo ambayo yanahitaji kushughulikiwa mapema zaidi tena chini ya Katiba sasa ni suala zima la kuwapo kwa Muungano.
Kati
ya matatizo ambayo tayari tumeyaona na yalikuwa yanatabirika sana tu ni
nafasi ya Zanzibar katika Muungano wa sasa na nafasi ya Tanganyika
katika Muungano mpya.
Haya mawili yamekuwa sehemu ya matatizo
yetu ya kisiasa kwa muda mrefu sasa na wakati umefika yaamuliwe mapema
zaidi na ikiwezekana kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2015.
Suala la
Muungano limekuwa tatizo kwa muda mrefu kwa sababu ya Zanzibar. Wakati
umefika kwa Wazanzibari kuamua kama wanataka kuwa sehemu ya Muungano na
Tanganyika.
Tokea mwanzo kabisa wa Muungano wetu Zanzibar imekuwa
ikipewa upendeleo na nafasi ya pekee kulinganisha na Tanganyika. Kwa
Watanganyika wengi uwepo au kutokuwepo kwa Zanzibar katika Muungano si
hoja nzito kwao.
Lakini uwepo wa Tanganyika kwa nchi ya Zanzibar
ndani ya Muungano ni jambo kubwa. Hofu ile ambayo ilikuwepo toka mwanzo
kwamba katika Muungano itaonekana Tanganyika imeimeza Zanzibar
imeshatimia na imekuwa kweli.
Hoja zote tunazosikia kuhusu
“Mamlaka Kamili” na “Zanzibar Kwanza” yote ni matokeo ya ukweli huu kuwa
Zanzibar inajihisi au angalau tuseme lipo kundi linaloamini Zanzibar
imemezwa na Tanganyika na sasa wanataka kujitoa katika koo hilo.
Kama
hili ni kweli au la ni Wazanzibari tu wanapaswa kuamua. Ni maoni yangu
kuwa wakati umefika kwa Wazanzibari kama walivyofanya kwenye suala la
Serikali yao ya “Umoja wa Kitaifa” na mabadiliko ya Katiba yao waanze
kudai mapema iwezekanevyo si tena “mamlaka kamili” bali “Kura ya Maoni”
ili kujitoa kwenye Muungano.
Wao tayari wana vyombo vyote vinavyoweza kusimamia hili na sioni sababu ya msingi kwanini wasifanye hivyo.
Imetosha
kusikia malalamiko na manung’uniko. Wazanzibar wadai wapatiwe nafasi ya
kupiga kura ya maoni kama wanataka kuendelea kuwa sehemu ya Muungano au
la.
Kama watasema hawataki basi uwekwe utaratibu ni lini na
tarehe gani Zanzibar itarudi na kuwa nchi huru yenye mamlaka kamili
(secede from the Union). Hili litasaidia hata siasa za Tanganyika kwani
mazungumzo ya Tanganyika yataacha kufikiria namna ya kuwaridhisha
Wazanzibari na badala yake watazungumzia namna ya kuipatia Tanganyika
Katiba yake na vyombo vyake vya utawala ambavyo vingi kama si vyote viko
katika “Serikali ya Muungano” hivi sasa.
Haya ni mambo makubwa
na ya msingi kutokea na yanapaswa kutokea mapema iwezekanavyo. Hii ni
pamoja na mabadiliko ya msingi ya Katiba ya sasa ili kusaidia michakato
mbalimbali ya kisiasa katika mazingira bora kama katika Tume ya
Uchaguzi, Sheria ya Vyama siasa n.k.
Tukifikia huku basi tutakuwa
tumefika mahali pazuri na nina uhakika tutarahisisha sana kazi ya
kuandika Katiba mpya – ama iwe ya Muungano au ya Tanganyika – huko
mbele. Tufanye mambo ya msingi kwanza.
Makala hii imenukuliwa kutoka gazetini: Raia Mwema
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment