Tuesday, 9 September 2014

Wenye ulemavu wa akili waruhusiwe kupiga kura kwenye chaguzi mbalimbali





Dodoma. Baadhi ya wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba wametaka
Katiba Mpya iwape haki ya kupiga kura katika chaguzi mbalimbali watu
wenye ulemavu wa akili lakini wana uwezo wa kujitambua.

Mapendekezo hayo mapya katika sura ya 12
yametolewa leo na Kamati namba saba wakati ambapo kamati mbalimbali
zimeendelea kuwasilisha taarifa za mapendekezo yao katika sura za 12, 13
na 16.
Akiwasilisha maoni ya kamati hiyo, bungeni mjini
Dodoma, Mjumbe wa kamati hiyo, Askofu Amos Mhagache amesema kamati yake
imependekeza pamoja na mambo mengine, kubadilishwa tafsiri ya neno akili
timamu ili kujumuisha watu wenye ulemavu wa akili lakini wanajitambua.

“Kuongeza ibara ndogo mpya itakayotoa tafsiri ya
maneno ‘akili timamu’ ambayo haitatafsiriwa kumnyima haki ya kupiga kura
mtu mwenye ulemavu wa akili,” alisema Askofu Mhagache.
Kwa upande wake mbunge wa Mpanda Mjini ambaye ni
mjumbe wa kamati namba kumi aliibua tena suala la muundo wa serikali
tatu kama ilivyopendekezwa na Tume ya Warioba.

Arfi akisoma maoni ya wachache alipinga kufanyika
kwa mabadiliko ya vifungu vinavyolenga kuwepo kwa mfumo wa serikali
mbili, badala ya mfumo wa serikali tatu, kama rasimu ya katiba
ilivyopendekeza.
Sura nyingine zilizowasilishwa pamoja na
mabadiliko yake, ni pamoja na sura ya 13 inayohusu taasisi za
uwajibikaji, ikiwamo Tume ya Maadili ya Uongozi na Uwajibikaji pamoja na
Tume ya Haki za Binadamu na sura ya 16 inayohusu mambo mengineyo. Chanzo MWANANCHI

Hongera UKAWA. Hakuna kurudi nyuma tena - Mwl Lwaitama

Maoni ya Mwalimu Lwaitama kuhusu maamuzi yaliyofikiwa katika mkutano baina ya Rais Kikwete na Wajumbe wa TCD.
Hongera UKAWA kwa kufanikisha hili lakini kazi bado mbichi!. Bado ni lazima kuelewa kuwa makubaliano haya yamehalalisha kuwepo kwa Rasimu mbili za Katiba inayopendekezwa, ile iliyowasilishwa Bunge Maalum na Jaji Warioba kwa niaba ya Tume ya Rais ya Mabadiriko ya Katiba kama Rasimu ya Pili ya Tume hiyo ya Rais na Rasimu ya CCM itakayotokana na Bunge Maalum lilosusiwa na UKAWA kuendelea hadi tarehe 4 Oktoba kuchakachua maudhui ya kimapinduzi yaliyomo katika Rasimu ya Pili iliyotayarishwa na Tume ya Rais.

UKAWA sasa tekelezeni dhana ya 'UKAWA ndio mpango mzima' !!! Lazima
kuwaeleimisha na kuwahamazisha wananchi kukataa Rasimu ya CCM (iliyosheheni mambo ya ajabu ya Bunge 3 Serikali 2!)) na kuhakikisha kuwa Serikali Kuu ya na Bunge la Jamhuri ya Muungano litakalopatikana baada ya Uchanguzi wa Oktoba 2015 itakuwa Serikali na Bunge litakalo kuwa limesheheni wanasiasa wenye nia dhabiti ya kujadili, kuboresha na kupitisha Rasimu ya Pili ya Katiba iliyowasilishwa Bunge Maalum na Jaji Warioba kwa niaba ya Tume ya Rais ya Mabadiliko ya Katiba iliyoongozwa na Jaji Warioba.

Lazima Bunge litakalo patikana baada ya Uchanguzi Mkuu wa 2015 liwe Bunge litakalo rekebisha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ili kuruhusu Wajumbe wa Bunge Maalum kuwa nusu theluthi moja wanasiasa na theluthi mbili wajumbe waliochanguliwa na makundi husika ya kiraia kuingia Bunge Maalum na Tume ya Rais ya Mabariko ya Katiba iliyoongozwa na Jaji Warioba kuendelea kusimamia mchakato wa katiba ndani ya Bunge Maalum na wakati wa upigwaji wa kura ya maoni ( kwa kutoa elimu ya uraia) hadi katiba mpya ipatikane. hongera UKAWA. Hakuna kurudi nyuma tena. Umoja wa vyama vya NCCR, CUF na Chadema utabadilisha siasa Tanzania kiasi kikubwa na ukiritiba wa chama kimoja, chama dola, kisiasa, utakomeshwa.
Mwl. Lwaitama
Maoni ya Mwalimu Lwaitama akiwaandikia Wanazuoni (kundi pepe la majadiliano). Chanzo WAVUTI

Uamuzi mgumu,Rais hataongeza muda Bunge la Katiba



Dodoma. Makubaliano baina ya Rais Jakaya Kikwete na viongozi wa Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD), kutaka Bunge Maalumu lifikie ukomo Oktoba 4, mwaka huu yamezua sintofahamu mjini hapa huku uamuzi huo ukionekana kuwachanganya viongozi wa Bunge hilo.
Kutwa nzima ya jana, viongozi wa Bunge Maalumu walishinda kwenye vikao vya mashauriano huku wabunge wa CCM wakitarajiwa kukutana jana usiku kwenye makao makuu ya chama hicho kupewa taarifa rasmi za uamuzi huo.
Katika makubaliano baina ya TCD na Rais Kikwete, imeamuliwa kuwa uamuzi wa Rais kupitia Tangazo la Serikali (GN) 254 la kuongeza siku 60 hadi Oktoba 4 uheshimiwe na baada ya tarehe hiyo Bunge liahirishwe.
Uamuzi huo ni kinyume cha azimio la Bunge Maalumu la Agosti 5, 2014 ambalo lilirekebisha Kanuni ya 14 (4) na kuifuta Jumamosi katika siku zilizotajwa kuwa za kazi, pia sikukuu na siku za Jumapili.
Mwenyekiti wa Bunge, Samuel Sitta alikaririwa akiwaambia wajumbe wa Bunge hilo kwamba Rais alikuwa ameridhia kwamba siku 60 alizotoa hazingejumuisha Jumamosi, Jumapili na siku za sikukuu.
Ni kwa msingi huo, Bunge hilo likapanga kwamba lingeendelea na shughuli zake hadi Oktoba 31, wakati Mwenyekiti wa Bunge atakapokabidhi Katiba inayopendekezwa kwa Rais Kikwete.
Hata hivyo, makubaliano yaliyofikiwa baina ya viongozi wa TCD na Rais yanaonekana kuvuruga kabisa ratiba ya Bunge hilo ambalo jana na juzi, Kamati ya Uongozi ilikutana mara kadhaa kuona jinsi ya kunusuru mchakato huo.
Ingawa haikufahamika mara moja kama vikao hivyo vya kamati ya uongozi inayoongozwa na Sitta mwenyewe vinajadili nini, lakini taarifa zimedai huenda kukawa na mabadiliko makubwa ya ratiba.
Habari nyingine zinadai kwamba mabadiliko hayo huenda yakapunguza muda wa baadhi ya shughuli za kazi za Bunge hilo ili liweze kukamilisha kazi yake ikiwamo wajumbe kupiga kura ya uamuzi.
Katika kikao cha jana asubuhi, kamati hiyo ilishindwa kurekebisha ratiba yake ili iendane na siku zilizosalia, hivyo kuahirishwa kwa kuwapa kazi wataalamu wake kuleta mapendekezo ambayo yangejadiliwa jana mchana.
Katibu wa Bunge Maalumu, Yahya Khamis Hamad alithibitisha jana kwamba ratiba ya Bunge imebadilika kutokana na hoja nyingi kukubalika ndani ya kamati.
“Kamati ya uongozi itakutana baadaye (jana) kuangalia vipengele ambavyo hawakukubaliana kwenye kamati ndivyo wavipangie muda na ratiba itajulikana baada ya kikao hicho,” alisema Hamad.

Hofu ya akidi
Hata hivyo, habari zaidi zinadai kwamba uongozi wa Bunge Maalumu ulichanganywa na kuwapo kwa hoja za baadhi ya wajumbe wake kutaka kwenda Makka kwa ajili ya kushiriki Ibada ya Hijja, hali inayotishia akidi kwa ajili ya kuendesha vikao.
Kanuni za Bunge Maalumu zinataka kuwapo kwa nusu ya wajumbe kutoka pande zote za Muungano wakati wa kuendesha vikao vyake na theluthi mbili ya wajumbe hao kila upande wakati wa kufanya uamuzi au kupiga kura.
“Tumetoka kwenye kikao mchana huu na pengine tutaitana tena maana hatujafikia mwafaka, kuna mambo mengi yamejitokeza lakini kubwa ni hili la wenzetu ambao wanataka kwenda Hijja, kuondoka kwao kunaweza kuathiri akidi kwa kiasi kikubwa,” kilisema chanzo chetu kutoka ndani ya kamati hiyo.
Kutokana na matakwa hayo, hivi sasa Ofisi ya Katibu wa Bunge inafanya tathmini ili kufahamu idadi ya wajumbe ambao watakwenda Hijja Septemba 22, mwaka huu, ambao wengi wanatoka Zanzibar.
Hamad alikiri kwamba kuna mambo mengi ambayo ofisi yake inayafanyia kazi na kwamba hilo la Hijja ni mojawapo... “Kwa sasa siko katika nafasi ya kuzungumza kwa kirefu, kikao cha Kamati ya Uongozi kimeisha na bado kuna kazi nyingi za kuona jinsi tunavyoendelea.”
Tayari Bunge hilo limetikiswa na kutokuwapo kwa wajumbe waliosusia vikao tangu Aprili 16, mwaka huu ambao ni wajumbe wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) ambao unaundwa na vyama vya CUF, Chadema na NCCR Mageuzi na baadhi kutoka Kundi la 201.

Taarifa ya TCD
Jana saa 7:00 mchana, Mwenyekiti wa TCD, John Cheyo alikutana na wanahabari na kueleza kuwa katika mazungumzo yao na Rais wamekubaliana mambo matano ya msingi kwa mustakabali wa nchi.
Alisema pamoja na kazi ya msingi iliyofanywa na Bunge Maalumu, mchakato unaoendelea hauwezi kutoa Katiba Mpya ambayo itatumika katika Uchaguzi Mkuu wa 2015.
“Muda hautoshi kukamilisha mchakato na kufanya mabadiliko yatakayohitajika ya sheria, kanuni na taasisi mbalimbali zinazohitajika,” alisema Cheyo ambaye pia ni Mbunge wa Bariadi Mashariki (UDP).
Alisema kura ya maoni ilipangwa kufanyika Aprili 2015 na kama itabidi irudiwe, basi itabidi irudiwe itakuwa Juni au Julai 2015, muda ambao Bunge la Jamhuri linatakiwa livunjwe.
“Ili Katiba Mpya itumike katika Uchaguzi Mkuu wa 2015, itabidi uhai wa Bunge na Serikali uongezwe zaidi ya 2015, jambo ambalo sisi viongozi wote hatuliungi mkono,” alisema Cheyo.
Alisema kwa kutambua kuwa kama kura ya maoni ikifanyika, italazimisha Uchaguzi Mkuu wa 2015 kuahirishwa, wamekubaliana kura hiyo iahirishwe hadi baada ya uchaguzi huo.
Bunge Maalumu 
Cheyo alisema Bunge Maalumu kwa sasa linafanya kazi kwa mujibu wa Tangazo la Serikali (GN), namba 254 lililotolewa na Rais Kikwete ambalo uhai wake utakoma Oktoba 4.
“Inategemewa kuwa Oktoba 4 Katiba inayopendekezwa itapatikana. Tulikubaliana hatua hii iachwe ifikiwe na baada ya hapo Bunge liahirishwe hadi baada ya Uchaguzi Mkuu 2015.
“Tarehe 4 Oktoba ndiyo mwisho. Hiyo ndiyo sheria iliyopo, sisi hatuna mamlaka ya kuandika GN mpya, GN imetolewa na Bunge hili liko kihalali. Tulichokuwa tunabishana lisife kesho,” alisema.
Akijibu maswali ya wanahabari kama ana uhakika Bunge hilo litaweza kukamilisha kazi yake ndani ya siku zilizobaki, Cheyo alisema “Tumeheshimu sheria iliyopo tarehe nne Watanzania wanategemea Katiba Mpya itakuwa imepatikana, sasa kama haitapatikana hilo msiniulize kwa sababu hilo si jukumu langu.”
Alipoulizwa kama rais ajaye baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 ataendeleza mchakato pale ulipoishia alisema: “Naomba Mungu rais ajaye awe anayejali maoni ya wananchi hilo naomba kabisa. Sasa tukipata rais ambaye hatutambui sisi wote na mawazo yetu, basi tutakuwa tumekosea katika kupiga kura.”

Mabadiliko ya 15 ya Katiba
Cheyo alisema kwa vile Uchaguzi Mkuu wa 2015 utafanyika kwa kutumia Katiba ya 1977, ni vyema yakafanyika mabadiliko madogo ili kuruhusu uchaguzi huru na wa haki.
Mabadiliko hayo yatalenga kuwezesha uwapo wa tume huru ya uchaguzi, mshindi wa urais ashinde kwa zaidi ya asilimia 50, kuruhusu mgombea binafsi na kuingiza ibara itakayoruhusu matokeo ya urais kupingwa mahakamani.
“Vyama vya siasa ambavyo vinapenda kupendekeza mambo mengine ya kurekebisha katika Katiba ya 1977 vinaombwa kufanya hivyo kwa vile muda tulionao ni mdogo,” alisema Cheyo.
Alisema walikubaliana kuwa marekebisho hayo yafanyike katika Bunge la Jamhuri litakaloanza Novemba 5 na ikishindikana yafanywe Februari 2015.

Ukawa kurudi bungeni
Cheyo alisema suala la kurudi au kutorudi ndani ya Bunge Maalumu la Katiba kwa wajumbe wa Ukawa halikuwa sehemu ya mkutano kati ya Rais na TCD.
“Kila siku nasema uamuzi wa vyama tuuheshimu. Wale wana sababu zao za kutoingia bungeni ni lazima tuheshimu msimamo wao kwa sababu wanazo sababu,” alisema. Chanzo MWANANCHI

Monday, 8 September 2014

Zitto: Wapambe wametufitini na Mbowe


Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe akifafanua jambo. Picha na Edwin Mjwahuzi  

Dar es Salaam. Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe ameeleza tofauti yake na mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, akisema imesababishwa na watu aliowaita wapambe.
Zitto (37), ambaye alikuwa naibu katibu mkuu wa Chadema, alisema kuwa hata kuvuliwa nyadhifa zake ndani ya chama kulisababishwa na wapambe hao, lakini akasisitiza kuwa hana kinyongo tena kwa kuwa alishamwomba Mungu na sasa amesamehe kabisa.
Tofauti za wawili hao hazijawahi kutolewa hadharani licha ya mitandao mbalimbali kuzungumzia kuharibika kwa uhusiano wao ikinukuu habari kutoka vikao vya ndani vya Chadema.
Hata hivyo, mapema mwaka huu, Zitto alirushiwa tuhuma nzito na Chadema kutokana na uhusiano wake na baadhi ya makada wa CCM, lakini mbunge huyo aliyahusisha maneno hayo na mwenyekiti wake na aliandika maneno makali dhidi ya Mbowe kwenye ukurasa wake wa facebook.
Lakini katika mahojiano na Mwananchi yaliyofanyika wiki iliyopita nyumbani kwake Masaki jijini Dar es Salaam, Zitto alionekana kujutia kuharibika huko kwa uhusiano wao na kusema “wapambe ndiyo wanatugombanisha”.
“Sina shida yoyote na Mbowe, naamini ipo siku tutagundua wapambe walituathiri na ndiyo waliotufikisha hapa,” alisisitiza Zitto bila kutaja ni kina nani hasa.
Zitto alisema yeye na Mbowe wametoka mbali tangu akiwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na hafurahii uhusiano wao ukiishia katika hali hiyo.
“Naumia sana, lakini naamini ipo siku ama nikiwa hai au nimekufa watu wataujua ukweli,” alisema mwanasiasa huyo kijana aliyepata umaarufu kutokana na uwezo wake wa kujenga hoja.
Alisema, akiwa mwenyekiti wa Serikali ya wanafunzi wa Chuo Kikuu (Daruso) yeye na mwenyekiti wake ndiyo waliokijenga chama wakati huo Mbowe akiwa mbunge wa Hai.
Alisema wakati huo Mbowe alikuwa akienda chumbani kwake kusuka mikakati ya kuiinua Chadema na kwamba walikuwa wakila chips pamoja na wakati mwingine kwenye klabu ya usiku ya Bilicanas inayomilikiwa na Mbowe.
“Wakati mwingine naangalia, naumia sana. Wakati tunafanya hayo yote wengine walikuwa CCM, wengine walikuwa wafanyabiashara, lakini sasa ndiyo wana sauti katika chama,” alisema Zitto.
Zitto alisema kuwa wakati huo walikuwa na kampeni yao waliyoiita ‘Real Madrid’ ambayo ilikuwa na lengo la kuingiza kila mwanasiasa bora katika chama chao.

Real Madrid ni klabu ya soka ya Hispania yenye mafanikio makubwa duniani na sera yake ni kusajili wachezaji nyota duniani kwa gharama zozote.
“Na kweli tulifanikiwa na kuongeza wabunge kutoka watano hadi 48 wa sasa,” alisema.
“I real miss that (nakumbuka sana). Naumia sana, mimi leo sina maelewano na watu ambao tulikuwa nao katika mapambano. Lakini nasononeshwa zaidi na kitu kinachoendelea ndani ya Chadema.
“Nini kimetokea Chadema? Kwa nini tumejikuta tumeondoka katika mstari? Tupo wabunge 48 bungeni sasa, lakini hatusogezi mbele nchi, tumerudi nyuma wakati huo tulikuwa watano lakini tulikuwa tunaenda vizuri sana.”
Akizungumzia jinsi wapambe walivyoharibu uhusiano wao, Zitto alisema kuna siku Mbowe alimtuhumu kuwa ameanzisha chama cha umma, pia akasema ana majina mawili tofauti katika mtandao wa Jamii forums ambayo anayatumia kuwasema viongozi wa Chadema.
“Kukatokea vurugu, baadaye nikasema naondoka. Ile nataka kutoka wabunge wakanizuia mlangoni nisipite, waliponizuia nilikuwa na hasira sana, nikawaambia lazima nitoke. Waliponizuia hasira zikanipanda nikaanguka chini nikalia sana, yaani sana” alisema akionekana mwenye hisia huku machozi yakimlengalenga.
Kwa mujibu wa Zitto, jioni ya siku hiyo walijikuta wamekaa meza moja na Mbowe na baada ya kuzungumza waligundua kuwa walikuwa wamelishwa maneno.
“Tulizungumza na wote tulilia sana. Wakati kama huu nikikumbuka nasikia uchungu kwa sababu ni wapambe wametufikisha hapa,” alisema.
Hata hivyo, Zitto alisema kuwa migogoro ni sehemu ya maisha na kwamba yeye anachukulia kama changamoto kwa kuwa hakuna njia inayonyooka moja kwa moja na hiyo ni sehemu ya kuendelea kumkomaza.
“Mmoja wa viongozi ambao ni role model wangu ni aliyekuwa Waziri Mkuu wa Malaysia, Mahathir Mohamad ambaye kila mwezi Oktoba huwa nakwenda Malaysia kuonana naye.
Mwaka jana wakati vurugu hizi zimeanza kushika kasi, watu wakaniambia unaweza vipi kukabili mambo kama haya, ila Mahathir ambaye alifukuzwa kwenye chama chake akiwa mbunge na baadaye akaja kuwa Waziri Mkuu, aliniambia hizi ni changamoto ambazo lazima upite,” alisisitiza Zitto.
Aliongeza kuwa hata Makamu wa Rais wa Kenya, Raila Odinga, alionana naye mwanzoni mwa mwaka na akamshauri asikate tamaa na kumweleza kuwa yeye hajafikia hata robo ya changamoto ambazo amepitia.

“Kwangu mimi changamoto hizi ni kukomazwa na sizungumzii kuonewa au kutoonewa, what I know (ninachojua) ni kwamba sijafanya kosa lolote na kwangu mimi nimesamehe na sina kinyongo na mtu yoyote.”
Mwaka huu baada ya msiba wa mama nimekwenda Umra Maka nimemuomba Mwenyezi Mungu na nimetoa vinyongo vyangu vyote na nimesema I have to move on (sina budi kusonga mbele) katika maisha yangu, sina chuki na tatizo na mtu.
“Huwezi kujua huko mbele mtakutanaje, just few months ago (miezi michache iliyopita) wabunge wa Chadema waliwaambia wabunge wa CUF kuwa ni mashoga, lakini leo ni marafiki.
Alikuwa akirejea kauli ya Chadema kuwa CUF ni mwanachama wa taasisi ya kimataifa ya kiliberali ambayo moja ya misingi yake ni kutetea usagaji, ushoga na ndoa za jinsia moja.
“Hivyo ndivyo ninavyoiona na huko mbele usishangae kuona tunafanya kazi pamoja. Kwangu mimi nimeshasahau kila kitu nimelia Umra na kila kitu nimesamehe,” alisema.
Alipoulizwa sababu za kutomfuata Mbowe ili wayazungumze na kuondoa tofauti zao, Zitto alisema sasa hivi siyo muda wa kumbugudhi kwa sababu yuko bize na Ukawa na uchaguzi, lakini anachoamini kuwa hata kama yeye Mbowe hatutakuwa hai, ipo siku itagundulika kuwa huu mgogoro ulipikwa na wapambe tu.
Akizungumzia uhusiano wake na katibu mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa, mbunge huyo alisema kuwa alikuwa na ukaribu wa kikazi tu na katibu huyo kutokana na kuwa kiongozi wake bungeni.
Kutelekeza ofisi
Akijibu tuhuma za kutelekeza ofisi ya naibu katibu mkuu, mbunge huyo alisema kuwa hizo ni tuhuma kama tuhuma nyingine na kwamba alikuwa anafanya kazi zake kama kawaida na kuhudhuria vikao, lakini kuna taratibu za kikatiba za kushughulika na jambo kama hilo.
“Hamuwezi mkakaa miaka miwili siji ofisini halafu mnakurupuka na kusema tumemfukuza kwa sababu alikuwa haendi ofisini. Kuna taratibu za kikatiba kwa mtu ambaye hashughuliki na kazi za chama au vikao mfululizo.
Kwa nini taratibu hizo hazikutumika wakati hiyo ni justification (uthibitisho) za mambo ambayo yalitokea, ambayo nisingependa kuyarejea kama vilivyosema hapo mwanzo.” aliongeza.
“Kazi za siasa siyo za ofisini ni kazi za field na kazi za field nimezifanya kwa kuendesha Operesheni Sangara na matunda yake ni kupata wabunge wengi Kanda ya Ziwa.

“Ni justification (uhalalishaji) tu kwamba kuna kitu kimetokea unatafuta sababu tu na kwangu mimi ni jambo dogo sana. Muhimu zaidi ni wapi tumekitoa chama na kukifikisha na wengine wakifikishe mbele zaidi,” alisema na kuongeza:
“Mimi nilikuwa nafanya kazi zangu kama kawaida na nilikuwa na ushirikiano mzuri na katibu mkuu kama inavyotakiwa,” alisisitiza.
Kuhusu madai kuwa CCM ilimuomba kujiunga na chama chao baada ya mgogoro huo kutokea, Zitto alisema hawajawahi kumtaka kabisa.
“Moja ya vitu ambavyo nashutumiwa na wenzangu ni kwamba mimi natumiwa na CCM lakini haijawahi kutokea kiongozi yeyote wa chama hicho, licha ya kuwa na uhusiano nao mzuri, kunitaka nijiunge nacho.
“January Makamba, Deo Filikunjombe, Kangi Lugola ni baadhi ya marafiki zangu walioko CCM lakini si vibaya kwa sababu hata watu wa Chadema wana marafiki ambao wapo CCM na wapo ambao wanaishi pamoja,” alisema Zitto.
Alisema mke wa Dk Slaa alikuwa diwani wa CCM lakini halikuwa tatizo, ila kwa Zitto kuwa na marafiki CCM lilikuwa tatizo.

Kujiunga chama kingine
Kuhusu kujiunga na chama kingine cha upinzani, Zitto alisema kuna vitu ambavyo unapokuwa kiongozi huwezi kuviweka wazi kwani kuna mazungumzo na watu ambayo ameyafanya lakini hawezi kuyatoa.
“Niishie kusema kwamba viongozi wengi sana nimezungumza nao. Wapo walionipa pole kwa yaliyonikuta na wengine kuniomba niungane nao, lakini sikuona sababu ya kutoka chama hiki kwenda chama kingine. Utapata faida ya siku mbili tatu katika kurasa za mbele za magazeti kuwa Zitto kaingia chama fulani lakini hutapata sustainable benefit (manufaa ya kudumu)” alisema.
“(Wilfred) Lwakatale alitoka CUF na kwenda Chadema, lakini hivi sasa wanafanya kazi pamoja. Kafulila katoka Chadema kaingia NCCR, Chadema wakamshambulia kuwa ni sisimizi lakini leo Kafulila ni shadow minister (waziri kivuli) chini ya Mbowe.”
Aliongeza kuwa hizo yeye anaona ni siasa nyepesi, kwa kuwa ana ndoto ya kuona nchi inabadilika na inabadilika kwa watu wanyonge na watu ambao leo hii hawana matumaini. Alisema kwa muda mrefu wananchi wanavumilia kuwa Watanzania, lakini hawajivunii kuwa Watanzania. Ndiyo maana katika ubunge wake ana kazi ya kuibua mambo mazito ili yafanyiwe kazi.
Akizungumzia mambo ambayo anaamini alifanikiwa katika maisha yake, Zitto alisema kuwa ni Bunge la 2005 hadi 2010 ambalo alizungumzia suala la madini kuhusu Buzwagi mpaka sheria mpya ya madini ikapatikana mwaka 2010.

“Leo hii katika tanzanite, Serikali inamiliki asilimia 50 kwa sababu ya sheria mpya. Pia Stamico ina hisa katika migodi na hii ilitokana na hoja za Buzwagi,” alisema Zitto ambaye ana shahada ya uchumi.
“Nilisimama bungeni kuzungumzia madini na siyo kuwa kulikuwa hakuna wabunge, lakini walikaa miaka mingi bungeni na hawakuona kuwa madini ni tatizo.
Nilichekwa na kuonekana sina maana lakini Rais aliunda Tume ya Bomani na watu wakaniambia nisiingie katika hiyo Tume lakini kwa mara ya kwanza ripoti ya Bomani ndiyo ripoti pekee iliyojadiliwa bungeni kati ya ripoti zote zilizoundwa kwenye sekta ya madini.”
Alisema kuwa katika Bunge la 2010 na 2015 alianza vibaya na hoja yake ya kuinua zao la mkonge ilikataliwa. Lakini hakuchoka na Aprili 2012 ripoti ya CAG ikatoka na akiwa mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) alitaka waliohusika kuwajibika na ndiyo akaibua hoja ya kutokuwa na imani na waziri mkuu na mawaziri wanane wakafukuzwa.

Kujiunga ACT
Alipoulizwa kuhusu mipango ya kujiunga chama kipya cha ACT, Zitto alisema pamoja na kwamba kauli yake kwamba atakuwa wa mwisho kuihama Chadema iko palepale na ndiyo maana ameenda mahakamani kutetea uanachama wake, kuna mambo matatu ya kuzingatia:
Moja, “viongozi wa ACT ni marafiki zangu na ni washirika wangu na falsafa (ideology) ya ACT ndiyo aidiolojia ninayoiamini ambayo ni ujamaa na tatu mimi ni mwanasiasa na hapa Tanzania mpaka sasa ili ufanye siasa lazima uwe kwenye chama cha siasa.”
Kutokana na matokeo ya mahakamani yatakavyokuwa kwa vyovyote vile Watanzania watarajie kuniona katika siasa na katika chama cha siasa ila hawataniona CCM.
“Siwezi kung’ang’ania kama wenzangu wa Chadema hawataki kuwa na mimi.
Lakini nafuatilia kwa karibu shughuli zinazofanywa na ACT na mimi siasa zangu ni hoja, ndiyo maana hamnioni nagombana wala natukana mtu na mkisikia Zitto mtasikia katika hoja na ACT wanajenga siasa za hoja.
“Wanaoongoza ACT ni watu ambao ninawaamini na haitakuwa jambo la ajabu itakapobidi kuwa nao, lakini cha msingi sasa hivi ni kwamba tuna kesi na leo mwanasheria wangu alitakiwa kuwasilisha majibu na tunasubiri hatima ya kesi ambayo ufafanuzi mkubwa ni kupata jibu la, hivi mtu anaweza kukurupuka tu na kumfukuza uanachama mtu bila kufuata taratibu zinazotakiwa?
Nikiiacha kesi bila kupata uamuzi, kuna watu wengi zaidi watakuja kuumia kwenye uamuzi wa aina hii.”

Alisema lazima mahakama itoe uamuzi kwamba taratibu za chama chenu ni hizi, zifuateni mzimalize, hamna sababu za haraka za kumnyonga mtu. Jaji mmoja alisema huwezi kumnyonga mtu halafu baadaye ndiyo unataka ajibu mashtaka.

Mabilioni ya Uswisi
Kuhusu mabilioni ya Uswisi, Zitto alisema kwa mara ya kwanza kwa nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara, Bunge la Tanzania lilikuwa la kwanza kupitisha azimio la kutaka masuala ya utoroshaji fedha yachunguzwe, likitokana na hoja yake.
Alisema uchunguzi wa mabilioni ya Uswisi bado unaendelea ingawa watu wanataka majina ila kwake majina si tatizo kwa sababu yataandikwa tu katika magazeti kwa siku mbili kama ambavyo ilitokea yalipotajwa majina ya mafisadi, lakini waliotajwa mpaka leo bado ni mawaziri.
“Mwaka jana nilikwenda kwenye mkutano Uingereza kumweleza Waziri Mkuu wa Uingereza kabla ya mkutano wa G8 nikiwa na Rakesh Rajan na leo hii kuna uchunguzi unaendelea.

Thursday, 4 September 2014

BAWACHA'S NEXT WOMEN'S CHAIRPERSON!

Sophia Mwakagenda Director at Tanzania Women and Youth Development Society donates water clothes and soap at Mwananyamala hospital. In her election campaigns as womens's chairperson at BAWACHA Sophia Mwakagenda visited Mwananyamala Regional hospital and offered support to patients and hospital staff.
Media listening to Sophia as she gives a word of speech to her supporters and fans at Mwananyamala hospital


Wednesday, 3 September 2014

MISINGI YA USAWA WA JINSIA IKILINDWA KATIKA KATIBA MPYA, TUTAPATA KATIBA YENYE MRENGO WA JINSIA

Baadhi ya Wajumbe wanawake wa Bunge Maalum la Katiba wakiimba kwa furaha wakati wa semina iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Pius Msekwa mjini Dodoma.
Makamu Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba (wa kwanza kulia) akipitia taarifa ya mapendekezo ya mtandao wa wanawake na Katiba Tanzania wakati wa semina iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Pius Msekwa mjini Dodoma.
Mjumbe wa Mtandao wa Wanawake na Katiba Bi. Usu Mallya akitoa mada kuhusiana na suala la kijinsia katika Katiba, wakati wa Semina iliyoandaliwa na Umoja huo kwa kushirikiana na Mtandao wa Wanawake na Katiba kwaajili ya Wajumbe wa Bunge Maalum kuhusu masuala ya Jinsia na Katiba iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Bunge wa Pius Msekwa Mjini Dodoma.

Usawa wa jinsia ni hali ya wanawake na wanaume kuwa na fursa sawa na upatikanaji wa haki zenye kuleta tija katika Nyanja mbalimbali za maendeleo ya jamii.Kati ya makundi haya mawili, lengo kuu la kuwepo kwa usawa wa jinsia ni kuhakikisha kuwa raia wote wanapewa nafasi ya kukua na kuondolewa vikwazo mbalimbali ili waweze kuchangia na kutambuliwa kwa usawa katika maendeleo yao ya kijamii, kiutamaduni, kiuchumi pamoja na kisiasa.

Ili Katiba iwe yenye mrengo wa jinsia hainabudi iwe inayotokana na mchakato uliyoshirikisha sauti za wanawake na wanaume wakati wa uandaaji wake na pia iliyoweka bayana makubaliano ya misingi mikuu itakayoongoza nchi ikibeba sauti zao.

Sambamba na hilo, Katiba hainabudi kuzingatia misingi ya demokrasia ikiwemo utawala wa sheria wenye kuwajibika kwa wananchi, usawa wa jinsia, utu na heshima ya kibinadamu kwa kila raia wakiwemo wanawake na wanaume, watoto wa kike na wa kiume.Aidha, Katiba iwe inayowezesha uwepo wa misingi mikuu ya usawa kati ya wanaume na wanawake katika vipengele mbalimbali vya Katiba.

Bila shaka twapaswa kujua kuwa Katiba ni‘Sheria Mama’ inayolinda haki za raia wote wakiwemo wanawake, wanaume na watoto nchini na kuainisha mfumo wa kuendesha nchi na wajibu wa viongozi wanaopewa dhamana ya kuongoza. Hivyo,ni vema Sheria hii Mama iwe imebeba masuala ama haki za makundi haya mbalimbali nchini kwa kudumisha maendeleo yenye tija.

Usawa wa jinsia ni msingi muhimu kwenye maendeleo ya nchi yeyote ikiwemo nchi yetu Tanzania, ambapo tafiti mbalimbali za hapa nchini na kwingineko zinaonyesha kuwa kwenye sekta ambazo zinatekeleza mipango yenye kulenga katika kukidhi mahitaji ya wanawake na wanaume pamoja na kutambua michango yao mbalimbali zimeleta tija zaidi kimaendeleo.

Ujenzi wa misingi ya usawa wa jinsia kwenye Katiba Mpya ni muhimu kwa kuwa Tanzania ni nchi mojawapo ya Afrika na Ulimwenguni ambayo imesaini Mikataba mingi ya Kimataifa na Kikanda ya kutekeleza Katiba, sera, sheria na mipango iliyojengewa kwenye misingi ya usawa wa jinsia nchini.

Mikataba hii inajumuisha Mkataba wa Kimataifa wa Kuondoa aina zote za Ubaguzi dhidi ya Wanawake (CEDAW), Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Watoto, Mpango wa Utekelezaji wa Mikakati ya Beijing, Protokali ya Makubaliano ya Haki za Binadamu na Usawa wa Jinsia ya Umoja wa Afrikapamoja na mikataba mingine kadha wa kadha.

Hivi karibuni, tumeona ama kusikia juu ya Semina iliyofanywa Bungeni mjini Dodoma na Umoja wa Wabunge Wanawake Tanzania (TWPG) kwa kushirikiana na Mtandao wa Wanawake na Katiba wakijadili juu ya umuhimu wa uwepo wa masuala ya jinsia katika Katiba Mpya na masuala muhimu ya jinsia ya kuzingatiwa katika katiba, ambapo wabunge hao waliweka mkazo katika suala zima la haki sawa katika Katiba kati ya wanawake na wanaume yani Hamsini kwa Hamsini.

Wabunge wanawake wa Tanzania wakishirikiana kwa pamoja na Mtandao wa Wanawake na Katiba waliweka bayana madai ya haki zao katika Katiba Mpyana madai haya ni kama ifuatavyo;-
Haki za wanawake zibainishwe kwenye Katiba Mpya, Sheria kandamizi zibatilishwe, Haki ya kufikia, kutumia, kunufaika na umiliki rasilimali ya nchi,

Utu wa mwanamke ulindwe, Utekelezwaji wa Mikataba ya Kimataifa kuhusu haki za wanawake, Haki sawa katika nafasi za uongozi, Haki za Wanawake wenye ulemavu, Haki ya uzazi salama, Haki za watoto wa kike, Haki ya kufikia na kufaidi huduma za msingi, Wajibu wa wazazi katika matunzo ya watoto pamoja na Katiba iunde chombo maalum kitakachosimamia haki za wanawake katika maeneo yote ya kijamii, kisiasa na kiuchumi.

Kimsingi, madai haya yote ya haki sawa yanayodaiwa na Wabunge hawa yana umuhimu mkubwa katika Katiba Mpya itakayopatikana kwani ndiyo yatayopelekea kupatikana kwa Katiba yenye mrengo wa jinsia.

Akitoa mada wakati wa semina hiyo, Mjumbe wa Mtandao wa Wanawake na Katiba Bi. Usu Mallya alisema kuwa suala la msingi wa usawa wa jinsia ni muhimu kuwekwa katika Katiba Mpya na baadaye kuwepo na uwajibikaji wake kwani kwa kufanya hivyo kutaipatia nchi katiba yenye mrengo wa kijinsia.

Bi. Mallya aliongeza kuwa wanawake wengi nchini wamekuwa hawapati fursa ya usawa wajinsia katika nyanja mbalimbali licha ya Tanzania kuwa kinara wa kutoa wanawake vinara ambao wamewahi kushika nyazifa mbalimbali na wengine bado wakiendelea kushika nafasi hizo za juu hapa nchini.

“Utafiti unaonyesha kuwa, asilimia 5% ya wanawake nchini ndiyo wanaomiliki ardhi, asilimia 39% ya wanawake hao hao hawapati elimu ya kutosha, pia utafiti unaonyesha kuwa asilimia 40.3% ya wanawake walioko kwenye ajira wapo katika sekta isiyo rasmi, wakati asilimia 10% ya Maprofesa wanawake ndiyo tunayo hapa nchini”, alisema Bi. Mallya.

Aidha, Bi. Mallya alizitaja changamoto mbalimbali zinazowakabili wanawake wengi nchini kuhusiana na usawa wa jinsia na haki zao pamoja na haki za watoto huku akitoa taarifa za utafiti zinazoonyesha kuwa mzigo wa kazi wa asilimia 66% ya wanawake wanafanya kazi zisizo na kipato, na asilimia 44% ya wanawake nchini walioolewa katika ndoa zao wamefanyiwa ukatili wa kijinsia.

Naye Mwenyekiti wa Women Fund Tanzania ambaye pia ni Mjumbe wa Mtandao wa Wanawake na Katiba, Profesa Ruth Meena alizungumzia juu ya masuala ya umuhimu wa jinsia ya kuzingatiwa katika Katiba Mpya huku akisisitiza juu ya usawa wa uongozi katika ngazi zote uwe hamsini kwa hamsini na uwepo wa chombo maalum kitakachozingatia haki za wanawake.

Profesa Meena alisisitiza kuwa kuna umuhimu wa Katiba Mpya iweze kulinda haki za watoto kwa kutoruhusu ndoa za utotoni, hivyo kuwepo na sheria zitakazo mlinda mtoto dhidi ya ndoa hizo mpaka mtoto anapotimiza umri wa miaka (18) Kumi na nane.

“Suala la umri wa mtoto wa kike kuolewa iwe ni miaka Kumi na nane, na mtu atakayeoa mtoto chini ya miaka kumi na nane awe amebaka”,alishauri Profesa Meena.

Aidha, Profesa Meena aligusia kuhusu masuala ya haki ya uzazi salama kwa wanawake pindi wanapojifungua, liweze kupewa kipaumbele kwa kujali usalama wa maisha ya mama na mtoto na isiwe hukumu ya kifo kwa akina mama.

“Iwe ni haki yetu ya uhai tunapofanya kazi ya kuongeza kizazi cha Tanzania, wanawake wapewe usalama wa uzazi wanapozaa pasipokuwa na kigugumizi, hivyo kuzaa kusiwe hukumu ya kifo kwa watoto wetu”,alisema Profesa Meena.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samia Suluhu Hassan ambaye pia alihudhuria katika semina hiyo, aliwatia moyo Wabunge wanawake hao na kuwataka kuwa na umoja wa kudai haki zao za usawa wa jinsia na alisisitiza juu uwepo wa ushirikiano kati ya wanaume na wanawake katika jamii.

Mhe. Samia hapa anawataka wanaume kuwaunga mkono wanawake kwa kuwapa nafasi za uongozi na waepuke tabia ya kuwadharau wanawake katika masuala mbalimbali yakiwemo uongozi ama kuwapa talaka kutokana kuwa na hofu, pindi wanawake wapatapo fursa ya uongozi.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Mhe. Sophia Simba naye ameitaka jamii kuwekea mkazo suala la elimu ya uzazi, kuwa ianze kutolewa kuanzia elimu ya msingi ili watoto waweze kuwa na uelewa wa kutosha pindi wanapokuwa wakubwa, Aidha alitoa hamsini kwa hamsini katika masuala yote katika jamii.

Kwaupande wawajumbe wengine wa Bunge hilo, Mhe. Hamad Rashid aliwashauri wanawake kuacha kutegemea Viti Maalum kwenye nafasi za ubunge kwa kuwa kufanya hivyo kutasaidia kujenga uwezo na kujiamini kuwa wanaweza.

“Mnapopata nafasi za uongozi mzitumie vizuri ili kuweza kujiamini na kujituma,” alisisitiza Mhe. Hamad. NayeWaziri Rajabu Salum mjumbe wa Bunge hilo, alisisitiza juu ya umuhimu wa elimu kuhusu masuala ya kijinsia yatolewe kwa msuguano, kwani wanaume wengi hawana uelewa wa jambo
hilo.

Agatha Senyagwa ambaye ni Mjumbe wa Bunge hilo, kutoka kundi la 201 upande wa wakulima, alisema ni vema elimu juu ya masuala ya kijinsia kwa wanawake wa vijijini ili nao wawe na uelewa kwa ajili ya kushiriki katika kugombea nafasihususan ngazi ya Serikali za Mitaa, mfano uwenyekiti wa kijiji na watendaji kata.

Ili kufanikisha uwepo wa Katiba hii yenye mrengo wa jinsia, hatunabudi kuingiza haki mahsusi (Gender specific) za wanawake na watoto wa kike katika Katiba, pia kuingiza misingi imara ya usawa wa jinsia na ile inayolinda haki za wanawake (Gender equality outcomes) katika vipengele mbalimbali vya Katiba.

(Picha zote na Benedict Liwenga, Maelezo-Dodoma).

Umoja wa Azaki za Vijana wakutana na Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba.

Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta akiongea na Umoja Azaki za Vijana wakati alipofanya mkutano nao wakati wakiwasilisha mapendekezo ya maboresho ikiwa ni msisitizo katika masuala yao ya vijana, mkutano uliofanyika 02 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa Spika Mjini Dodoma.
Baadhi ya Vijana wanaounda Umoja wa Azaki za Vijana wakisikiliza kwa makini maneno mazuri toka kwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba (hayupo pichani) wakati walipokuwa wakiwasilisha mapendekezo ya maboresho ikiwa ni msisitizo katika masuala yao ya vijana, mkutano uliofanyika 02 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa Spika Mjini Dodoma.
Baadhi ya Vijana wanaounda Umoja wa Azaki za Vijana wakisikiliza kwa makini maneno mazuri toka kwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba (hayupo pichani) wakati walipokuwa wakiwasilisha mapendekezo ya maboresho ikiwa ni msisitizo katika masuala yao ya vijana, mkutano uliofanyika 02 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa Spika Mjini Dodoma.
Baadhi ya Vijana wanaounda Umoja wa Azaki za Vijana wakisikiliza kwa makini maneno mazuri toka kwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba (hayupo pichani) wakati walipokuwa wakiwasilisha mapendekezo ya maboresho ikiwa ni msisitizo katika masuala yao ya vijana, mkutano uliofanyika 02 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa Spika Mjini Dodoma.
Baadhi ya Vijana wanaounda Umoja wa Azaki za Vijana wakisikiliza kwa makini maneno mazuri toka kwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba (hayupo pichani) wakati walipokuwa wakiwasilisha mapendekezo ya maboresho ikiwa ni msisitizo katika masuala yao ya vijana, mkutano uliofanyika 02 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa Spika Mjini Dodoma.
Baadhi ya Waandishi wa Habari wakiwa kazini kufuatilia mambo yakiyoendelea katika mkutano huo wa Umoja wa Azaki za Vijana uliofanyika 02 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa Spika Mjini Dodoma.
Kiongozi wa msafara wa Umoja wa Umoja wa Azaki za Vijana Alfred Kiwuyo (kulia) akikabidhi taarifa kwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta wakati wakiwasilisha mapendekezo ya maboresho ikiwa ni msisitizo katika masuala yao ya vijana, mkutano uliofanyika 02 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa Spika Mjini Dodoma. Picha zote na Benedict Liwenga, Malezo-Dodoma


Na Benedict Liwenga, Maelezo-Dodoma.
UMOJA wa Azaki za Vijana wakutana na Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta wakiwa na lengo la kuja kuwasilisha mapendekezo yao kwa ajili ya maboresho ya Rasimu ya Pili ya Katiba Mpya.
Akizungumza kwa niaba ya vijana wenzake, Kiongozi wa msafara huo Alfred Kiwuyo amesema kuwa Azaki hizo za vijana zilishiriki mchakato mzima wa Katiba katika hatua zote muhimu ikiwemo kukusanya maoni na kuyawasilisha mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Pamoja na ushiriki huo, Bw. Kiwuyo ameeleza kuwa sehemu kubwa ya maoni ya vijana yamejumuishwa katika kifungu cha 44 cha Rasimu ya Pili ya Katiba, na mjumuisho huo wa haki na wajibu wa vijana umefinya sana maoni ya vijana katika Rasimu hiyo.
“Lengo kuu la mtazamo huu sio kuleta hoja mpya, bali ni kuboresha Rasimu ya Pili ya Katiba Mpya na katika maboresho hayo tunapendekeza mambo matatu ya msingi, kwanza ni kuwekwa kwa tafsiri ya neno kijana katika Rasimu, kutenganisha haki na wajibu wa vijana na mwisho ni kuweka kifungu kitakacho wezesha kuundwa kwa Baraza huru la Vijana la Taifa”, alisema Kiwuyo.
Aidha, Kiwuyo ameongeza kuwa Azaki za vijana zinatambua kuwa haki ya uandishi wa Katiba ni ya kila Mtanzania na kwa utaratibu waliojiwekea wao wenyewe Wabunge wa Bunge Maalum la Katiba ndiyo wawakilishi wao katika hilo, hivyo wanamatumaini makubwa kuwa Katiba itaandikwa na Watanzania wa makundi yote wakiwemo na vijana.
Naye Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta amesema kuwa Ibara ya 44 katika Rasimu ya Tume inayuzungumzia mambo ya vijana imekuwa fupi na imeacha baadhi ya mambo muhimu zikiwemo haki ambazo hazikuelezewa vizuri, mambo ya haki na wajibu wa vijana na pia haijataja juu ya chombo cha uwakilishi cha vijana.
“Hii Ibara ya 44 katika Rasimu ya Tume imekuwa fupi na imeacha baadhi ya mambo muhimu, hivyo niwahakikishieni kuwa mawazo haya ya vijana tutawafikishia wahusika ambao ni Kamati ya Uandishi na Uongozi wa Bunge Maalum la Katiba ili yaweze kufanyiwa kazi, lakini pia suala la wajibu ambalo mmeliomba ni jambo zuri kwa ninyi vijana kwani ni muongozo”, alisema Mhe. Sitta.
Naye Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Paul Makonda amemshukuru Mwenyekiti wa Bunge hilo, kwa kupokelewa kwa vijana hao kama kundi kubwa katika jamii na amesisitiza juu ya Katiba kuwezesha kuundwa kwa Baraza Huru la Vijana la Taifa kwani litawezesha kuwaunganisha vijana nchini.
“Baraza kwetu ni jambo la msingi kwani litakuwa ni chombo kitakachotusaidia katika mambo ya uwakilishi kwa vijana nchini, kwani hivi sasa hatuna vijana wenye kuwakilisha vijana wenzao katika mambo mbalimbali kupitia chombo kama hiko, hivyo Katiba iweke kipengele kitakachowezesha kuundwa kwa chombo hiko”, alisema Makonda.
Makonda alisisitiza kuwepo na haki, wajibu na uwajibikaji kutasaidia kuwa na vijana waadilifu na wenye kuzingatia maadili.

Azaki za Vijana katika mchakato wa Katiba zinajumuisha Tanzania Youth Vision Association (TYVA), FEMINA, Restless Development, Tanzania Youth Coalition (TYC), Youth of United Nations Association of Tanzania (YUNA) pamoja na TAMASHA.